Na Doris Petro
KWAYA ya Chang’ombe Vijana (CVC), ambayo iko chini ya Kanisa la Africa Inland Church Tanzania (AICT), Ushirika wa Chang’ombe jijini Dar es Salaam Desemba 29, mwaka huu itaadhimisha miaka 25 tangu ianzishwe.

 Mwenyekiti wa kwaya hiyo, Elias Msula amesema kuwa, siku hiyo kutakuwa na ibada maalum ya shukrani ambayo itafanyika kuanzia saa mbili asubuhi. Alisema ibada hiyo itatawaliwa na kusifu na kuabudu. Ametoa wito kwa watu wote bila kujali madhehebu yao kuhudhuria ibada hiyo, ambayo pia itahudhuriwa na kwaya mbalimbali.

Alizitaja baadhi ya kwaya hizo kuwa ni AIC Dar es Salaam Kwaya, Ukombozi ya KKKT Msasani, AIC Shinyanga pamoja na kwaya wenyeji. Hata hivyo, amesema tukio hilo litatanguliwa na semina ya uimbaji ambayo itafanyika Jumamosi Desemba 28 kanisani hapo.

Alisema kuwa, katika semina hiyo waimbaji kutoka makanisa mbalimbali pamoja na Wakristo wote wanaalikwa kuhudhuria semina hiyo ambapo mada mbalimbali zitatolewa. Miongoni mwa mada zitakazotolewa kwa mujibu wa Msula ni “Uimbaji kama sehemu ya ibada na Waimbaji kujitambua kama Watumishi.” Alisema miongoni mwa watumishi wa Mungu watakaotoa mada katika semina hiyo ni Mchungaji Daniel Mgogo wa Kanisa la Baptist Mbeya.

Msula alisema tukio hilo litaenda sanjari na kuzindua rasmi programu ya ujenzi wa jengo la kitega uchumi cha kwaya hiyo katika eneo la Mtoni Kijichi. Aidha, alisema watauza cd yenye mchanganyiko wa nyimbo zilizomo katika matoleo 12 ya kwaya hiyo tangu ianzishwe.

Akizungumzia mafanikio ya kwaya hiyo katika kipindi cha miaka 25, Msula alisema kuwa, kwaya hiyo imekua kiroho na kiidadi. Alisema wakati kwaya inaanzishwa mwaka 1988 ilikuwa na wanakwaya 15 lakini sasa ina wanakwaya 90.


Kuhusu kukua kiroho, Msula alisema kuwa, kwaya imekuwa na maombi ya kufunga kila Alhamis ya mwisho wa mwezi pamoja na vipindi vya kujifunza neno la Mungu kila kabla ya kufanya mazoezi.

“Yapo mengi sana. Kwa mfano kwa miaka mitano kati ya mwaka 2007 na 2012 tumeshirikiana na  kanisa la AIC Ipagala mjini Dodoma kulijenga na kulikuza kwa kufanya mikutano ya Injili kila Agosti ya kila mwaka. Tulishuhudia nyumba kwa nyumba na kufanya maombezi. Tulipoanza waumini walikuwa hawazidi 20 lakini sasa kwa neema ya Mungu wako zaidi ya 200,” alisema na kuongeza:

“Mwaka 1999 kuelekea 2000 kwaya ya CVC tulifanya mikutano ya uinjilisti huko Eldoret nchini Kenya na watu wengi walimwona Mungu. Pia tumehusika na umisheni kwa kufanya injili katika eneo la Usandawi, ambalo ni miongoni mwa maeneo hapa nchini ambayo yalikuwa hayajafikiwa kwa injili kwa kiasi kikubwa. Kwa kipindi hicho pia tumeweza kuwa na mradi wa studio inayojulikana kama CVC Studio ambayo imetoa ajira kwa wanakwaya watano.”
                    
                            Mchoro wa jengo la kitega uchumi ambalo linatarajiwa kujengwa na CVC

Kwaya ya CVC imeendelea kuwa miongoni mwa kwaya zenye kupendwa na idadi kubwa ya wapenzi wa nyimbo za injili hasa kutokana na nyimbo za Gusa, Vunja, Usiku wa Manane, Mpinga Kristo na nyingine nyingi.   

0 comments:

Post a Comment

 
Top