Na Nestory Ngwega, Tanga

KATIKA hali isiyo ya kawaida kutokea kwenye mikutano ya injili,watumishi wa mhubiri mwenye jina kubwa nchini,  Mchungaji Josephat Gwajima wamemshambulia kwa kipigo kikali mwanafunzi wa chuo cha uandishi wa habari ambaye pia mshirika wa Kanisa la Assemblies of God (TAG), jijini Tanga,  Elias Mokiwa kwa kudaiwa kutenda kosa la kupiga picha misukule inayodaiwa kurudishwa kupitia maombi ya huduma hiyo.


Tukio hilo lililowashangaza watu wengi,  wakiwemo wasio Wakristo, lilitokea Jumapili Desemba Mosi, mwaka huu kwenye viwanja vya Tangamano wakati mhubiri Gwajima (pichani) akiwa anaendelea na mahubiri yake ya kuwaita misukule "njoooooo" akisisitiza kuwa kwa kuwaita vile misukule wangetoka waliko na kwenda mkutanoni pale.


Kupigwa kwa kijana huyo ambaye ni mwanafunzi wa chuo cha uandishi wa habari cha Royal kilichoko jijini hapa, kulitokana na kitendo chake cha kupiga picha mama mmoja aliyedaiwa kuwa ni msukule, ambaye alikuwa ameanguka mbele madhabahuni.

Elias aliwaambia waandishi wa habari kuwa, baada ya kukamatwa akipiga picha, alichukuliwa na kupelekwa nyuma ya jukwaa wakamvua mkanda ambao ulitumika kumfunga mikono yake yote miwili kwa nyuma na kisha kumpa kipigo kama mwizi.

"Nilishambuliwa kwa mateke ngumi na magongo..kwakweli najisikia maumivu sana. Tangu saa 12 jioni waliponikamata waliniachia saa mbli usiku nikiwa nyuma ya jukwaa mahali ambapo watu wengi walikuwa hawaoni tukio hilo isipookuwa mwanachuo mwenzangu mmoja anayeitwa Veronica Mboto ndiye aliyeshuhudia na kutoa taarifa iliyopekea baadaye kuokolea kutoka eneo hilo nililoliona kama kuzimu."alisema.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Constatine Massawe alipoulizwa kuhusu tukio hilo alisema kuwa yuko safarini. Hata hivyo, alisema kuwa kama kweli itathibitika watuhumiwa watachukuliwa hatua kama wahalifu wengine. Alimwambia mwandishi wa habari hizi kuwasiliana na mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai mkoa wa Tanga (RCO), Aziz Kimata.

Akizungumzia tukio hilo, Kimata alisema kuwa watachukua hatua baada ya upelelezi wa awali kukamilika.

Mchungaji Gwajima ambaye ni kiongozi mkuu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima hakuweza kupatikana kuzungumzia tukio hilo, hata waandishi walipojaribu kukutana naye walinzi wake waliwazuia. Hata simu yake ya mkononi pamoja na za wasaidizi wake wa karibu zilikuwa hazipatikani mwandishi wa habari hizi alipopiga.

Baadhi ya wakristo waliohojiwa na walionekana kushangazwa na tukio hilo, wakieleza kuwa  haijawahi kutokea kwa wahudumu wa mkutano wa injili kupiga watu kama ilivyotokea.

"Sisi wakristo ikitokea miujiza kwenye mkutano wa injili tunawaita waandishi wa habari waje watangaze kwani huo ni ushuhuda na watu wengine wajue kuwa Mungu wetu anaweza. ..sasa hawa wenzetu wanadai kufufua misukule ambao ni muujiza mkubwa halafu hawataki waandishi kuwapiga picha na kuwatangaza, tuna wasiwasi na miujiza hiyo kama ni misukule ya kweli au feki' alisema mtumishi mmoja ambaye hakutaka jina lake liandikwe.


0 comments:

Post a Comment

 
Top