Na Catherine Oguda, Dar es Salaam
WATU mbalimbali waliotoa maoni yao kufuatia mahubiri ya Askofu Mkuu wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF), Zachary Kakobe katika ibada ya Krismas aliyohubiri kanisani Mwenge jijini Dar es Salaam, wamempongeza na kusema ni kiongozi wa dini mwenye kuthubutu kukemea waziwazi.

Jacob Luhende, mkazi wa Kimara Mwisho alisema kuwa, kama viongozi wengi wa dini wangekuwa wanatimiza wajibu wao ikiwemo kukemea maovu, ana uhakika nchi isingefika hapa ilipo sasa.

“Baadhi ya viongozi wa dini wanatuangusha. Wanafunga ndoa na viongozi mafisadi. Kakobe anakemea viongozi wa ovyo, kama viongozi wetu wa dini wote wangekemea mfano wa Kakobe mimi ninaamini kuwa nchi yetu isingefika hapa tulipo sasa,” alisema.

Naye Judith Kalumuna, mkazi wa Mbezi Beach yeye alisema kuwa amekoshwa na ujumbe aliohubiri Askofu Kakobe. “Ukweli nimekoshwa sana na mahubiri ya Askofu Kakobe, yamenifariji pia. Unajua tunapoona viongozi wetu wa kiroho wanaungana na sisi wananchi tunaoumizwa kutokana na vitendo viovu vya baadhi ya watu waliopewa dhamana ya kuongoza, inatupa faraja sana.

Na mimi ninadhani kama viongozi wote wa dini, hasa wale ambao wana makundi ya watu wengi wanaoiwafanya wawe maarufu wangekuwa wanakemea uovu kwa uwazi bila kujipendekeza kwa watawala ingetusaidia sana,” alisema Judith.

Abdallah Juma, mkazi wa Mazense yeye alisema kuwa ingawa hajasoma kwenye magazeti wala hajasikia redioni au kwenye televisheni, lakini amesikia watu wakizungumzia mahubiri hayo alipokuwa kwenye daladala akiwa kwenye mizunguko yake.

“Ukweli mimi sijasikia wala kusoma nini alichosema huyo askofu kwenye mahubiri yake, lakini nimesikia kwenye daladala wakizungumzia hayo mambo. Kama kweli ndivyo alivyohubiri mimi nakubaliana naye, na ni vizuri viongozi wengine wa Kikristo na Kiislamu wakawa wanakemea maovu ya viongozi kila wakati,” alisema.

Akihubiri katika ibada hiyo, Askofu Kakobe alisema kuwa, wametokea baadhi ya wanasiasa hapa nchini ambao wanajiona ni miungu watu na kujaribu kuwazuia watu wengine hususani viongozi wa dini wasiongelee mambo ya siasa kwa kigezo kwamba eti Biblia inasema ya Kaisari mpe Kaisari na ya Mungu mpe Mungu, hivyo viongozi hao wa dini hawastahili kuongelea au kujihusisha na mambo ya siasa. 

Akifafanua alisema, “watu hao hawajui Biblia na wanajaribu kuwapotosha watu. Alisema Yesu aliwajibu wanafunzi wake baada ya kuulizwa juu ya uhalali wao (wanafunzi) wa kulipa kodi ya Kaisari wakati wao waliamriwa na Musa kulipa kodi ya Mungu. Ndipo akawajibu kwamba ya Kaisari wampe Kaisari na ya Mungu Wampe Mungu akimaanisha kwamba walipe kodi ya Kaisari na walipe kodi ya Mungu pia kama walivyo amriwa (Luka 20: 21-25; Hesabu 31: 25-39). Hivyo mimi kama mtumishi wa Mungu siwezi kuacha kukemea mahali penye uovu na nitapongeza panapostahili kupongezwa”.

Viongozi wa nchi na rasilimali zetu.

Alisema kuwa Tanzania ni nchi iliyobarikiwa sana kwa kuwa na rasilimali nyingi lakini wananchi wake ni maskini. Alisema, hiyo inatokana na kuwa na viongozi ambao hawana maono ya kuwaletea wananchi maendeleo badala yake wao wanajiangalia wenyewe na familia zao. 

Kakobe alisema kuwa, kutokana na hali hiyo ndio maana mtu akipata uongozi anasema "ameula". Alisema kiongozi bora ni yule mwenye kipaji cha kuzaliwa cha uongozi na sio vyeti vya darasani pekee. “Sio kila mtu anaweza kuwa rais wa nchi, ni lazima tuhakikishe tunamchagua kiongozi ambaye ana maono ya kututoa kutoka katika umaskini tulionao na kuleta maendeleo ya kiuchumi,"alisema.

Siasa za chumbani, siasa haramu.
Askofu Kakobe aliwataka wanasiasa na wananchi kwa ujumla kudumisha umoja badala ya kuleta siasa za chuki. Alisema wako baadhi ya wanasiasa ambao wamechoka kisiasa hivyo wanaleta propaganda za udini, ukabila na ukanda. "Watu wanadiriki hata kusema chama fulani ni cha dini fulani, eti hatutaki Rais atoke ukanda fulani. Hizi ni siasa haramu na wanaoeneza propaganda hizo nao ni haramu," alisema na kuongeza:

“Hatumchagui mtu au malaika wa kutupeleka mbinguni bali mtu wa kuifanya Tanzania kuwa nchi ya asali na maziwa kwa faida ya wananchi wote. Wanasiasa waache siasa za chumbani za kunyosheana vidole kuhusu ndoa zao. "Tusiendekeze siasa za chumbani,hatumchagui kiongozi wa kutupeleka mbinguni bali tunamchagua kiongozi wa kutuletea neema hapa hapa Tanzania.

 Watu leo wanamsifia Mandela kwamba alikuwa kiongozi bora lakini wanasahau kwamba Mandela huyuhuyu maisha yake ya ndoa yalikuwa na kasoro kubwa. Aliweza kuwasamehe makaburu lakini alishindwa kumsamehe mkewe Winnie. Ni nani Kiongozi wa nchi hapa Tanzania anaweza kusema yeye ni msafi? Kwani sisi hatujui maisha ya JK? Tuache siasa za chumbani, tuchague kiongozi bora.”

Aidha, Askofu Kakobe alishauri chama tawala na serikali kwa ujumla kukubali  uundwaji wa Tume Huru ya Uchaguzi ili kuondoa malalamiko kutoka kwa vyama vya upinzani.
Askofu huyo pia alishauri siku ya uchaguzi mkuu isiwe Jumapili, Jumamosi au Ijumaa bali serikali itenge siku yoyote katikati ya wiki ili wananchi wengi zaidi waweze kujitokeza kupiga kura.

0 comments:

Post a Comment

 
Top